Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Monday 20 March 2017

Hekima,Busara na Amani.;Muwe na mchana Mwema..




Anayeonywa mara nyingi akawa mkaidi, ataangamia ghafla asipone tena. Waadilifu wakitawala watu hufurahi, lakini waovu wakitawala watu hulalamika. Apendaye hekima humfurahisha baba yake; lakini aandamanaye na malaya hufuja mali yake. Mfalme akitumia haki huipatia nchi uthabiti, lakini akipenda hongo taifa huangamia. Mwenye kumbembeleza jirani yake, anatega mtego wa kujinasa mwenyewe. Mtu mbaya hunaswa kwa kosa lake, lakini mtu mwadilifu huimba na kufurahi. Mwadilifu anajua haki za maskini, lakini mtu mwovu hajui mambo hayo. Wenye dharau huutia vurugu mji mzima, lakini wenye hekima hutuliza ghadhabu. Mwenye hekima akibishana na mpumbavu, mpumbavu huwaka hasira na kucheka bila kutulia. Wapendao kumwaga damu humchukia mtu asiye na hatia, lakini watu wema huyalinda maisha yake. Mpumbavu huonesha hasira yake wazi, lakini mwenye hekima huizuia na kuituliza. Mtawala akisikiliza mambo ya uongo, maofisa wake wote watakuwa waovu. Maskini na mkandamizaji wanafanana kwa kitu kimoja: Wote wawili wamepewa macho na Mwenyezi-Mungu. Mfalme anayewaamua maskini kwa haki, atauona utawala wake umeimarika milele. Adhabu na maonyo huleta hekima, lakini mtoto aliyeachwa afanye apendavyo humwaibisha mama yake. Waovu wakitawala maovu huongezeka, lakini waadilifu watashuhudia kuanguka kwao. Mpe nidhamu mwanao naye hatakupa wasiwasi; yeye ataufurahisha moyo wako. Pasipo maono ya kinabii watu hukosa nidhamu; heri mtu yule anayeshika sheria. Mtumwa haonyeki kwa maneno matupu, maana ingawa anayaelewa yeye hatayatii. Wamwona mtu apayukaye bila kufikiri? Mtu mpumbavu ni afadhali kuliko yeye. Ambembelezaye mtumwa wake tangu utoto, mwishowe mtumwa huyo atamrithi. Mwenye ghadhabu huchochea ugomvi, mtu wa hasira husababisha makosa mengi. Kiburi cha mtu humporomosha mwenyewe, lakini mnyenyekevu wa roho atapata heshima. Anayeshirikiana na mwizi anajidhuru mwenyewe; husikia laana ya aliyeonewa bila kusema neno. Kuwaogopa watu ni kujitega mwenyewe, lakini anayemtumaini Mwenyezi-Mungu yu salama. Wengi hupenda kujipendekeza kwa mtawala, hali mtu hupata haki yake kwa Mwenyezi-Mungu. Mdhalimu ni chukizo kwa mnyofu, naye mnyofu ni chukizo kwa mwovu.
Methali 29:1-27
"Swahili Na Waswahili"Pamoja Daima.

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo43...

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Tumshukuru Mungu kwa kibali cha kuiona siku hii tena..

Asante Baba yetu, Mungu wetu,Mwokozi,Muumba wetu,Muumba Mbingu na nchi,Mungu wa Abrahamu,Isaka na Yakobo..Asante kwa kutuchagua na kutupa nafasi hii tena ya kuendelea kuiona leo hii..si kwa wema wetu,nguvu/utashi,ujuzi wetu Baba bali ni kwa Neema/Rehema zako..
Jana imepita Baba Leo ni siku mpya na kesho ni sikunyingine Mfalme wa Amani tunaomba utawale katika maisha yetu,Roho mtakatifu atuongoze kwenye kunena/kutenda,Ukabariki kazi zetu,Biashara,Masomo Baba,Hatua zetu ziwe nawe,Vyombo vya usafiri na tutembeapo,Tuingiapo/Tutokapo Baba ukawe nasi...
ukatakase vyote tunavyoenda kugusa/kutumia..Ukatutakase Miili yetu,Akili zetu  kwa damu ya Bwana wetu,Mwokozi wetu Yesu Kristo iliyo mwagika kwa ajili yetu..
Baba utusaheme pale tulipokwenda kinyume nawe.. Nasi utupe Neema ya kuweza kusameheana..
Baba ukwaponye/kuwaokoa wote wanaopitia Magumu/mapito,Shida/Tabu,Ukawafungue waliokatika vifungo mbalimbali vya mwovu..ukawaguse na kuwaweka  huru kiroho na kimwili..
Mafalme wa Amani utawale na kuilinda Nchi hii tunayoishi,Baba ukatawale Tanzania,Afrika na Dunia yote..

Ukawaongoze wanaotuongoza wakaongoze katika haki na kweli..

tunarudisha Sifa na Utukufu ni kwako Baba wa Mbinguni..
Tunajiachilia Mikononi mwako Tukiamni wewe ni Bwana na mwokozi wetu
Amina...!!!

Utajiri, hekima na elimu ya Mungu ni kuu mno! Huruma zake hazichunguziki, na njia zake hazieleweki! Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu: “Nani aliyepata kuyajua mawazo ya Bwana? Nani awezaye kuwa mshauri wake? Au, nani aliyempa yeye kitu kwanza hata aweze kulipwa tena kitu hicho?” Kwa maana vitu vyote vyatoka kwake, vyote vipo kwa uwezo wake na kwa ajili yake. Utukufu na uwe kwake hata milele! Amina.
Tuanze siku/wiki na Mungu...
Mungu aendelee kuwabariki.


Benyamini aenda Misri

1Kisha njaa ilizidi kuwa kali katika nchi ya Kanaani. 2Baada ya kile chakula walichokuwa wamenunua kutoka Misri kumalizika, Yakobo akawaambia wanawe, “Nendeni tena Misri, mkatununulie chakula kidogo.” 3Lakini Yuda akamwambia baba yake, “Yule mtu alituonya vikali, akisema, ‘Sitawapokea msipokuja na ndugu yenu mdogo.’ 4Kama utakubali ndugu yetu kwenda pamoja nasi, basi, tutakwenda kukununulia chakula. 5Lakini iwapo hutakubali aende nasi, basi, hatutakwenda huko, kwani yule mtu alituambia waziwazi, ‘Hamtaniona msipokuja na ndugu yenu mdogo.’” 6Israeli akasema, “Kwa nini mkanitia taabuni kwa kumwambia huyo mtu kwamba mnaye ndugu mwingine?” 7Wakamjibu, “Yule mtu alituhoji kwa makini sana kuhusu mambo yetu na jamaa yetu akisema, ‘Je, baba yenu angali hai? Je, mnaye ndugu mwingine?’ Hivyo tulimjibu kulingana na maswali yake. Tungaliwezaje kujua kwamba atatuambia, ‘Mleteni ndugu yenu?’” 8Yuda akamwambia Israeli, baba yake, “Niruhusu mimi niende naye ili tuondoke mara moja, tuende tukanunue chakula, tusije tukafa njaa pamoja nawe na watoto wetu. 9Mimi mwenyewe nitakuwa mdhamini wake. Wewe utanidai mimi. Nisipomrudisha ukamwona kwa macho yako mwenyewe, lawama na iwe juu yangu milele. 10Kama tusingalikawia, tungalikuwa tumekwisha kwenda na kurudi mara mbili.”
11Hapo Israeli, baba yao, akawaambia, “Haya! Kwa vile ni lazima iwe hivyo basi, fanyeni hivi: Chukueni katika mifuko yenu baadhi ya mazao bora ya nchi yetu, mkampelekee zawadi huyo mkuu. Mchukulieni mafuta kidogo ya mkwaju, asali kidogo, ubani, manemane, kungu na lozi. 12Chukueni fedha mara mbili ya ile inayohitajika, kwa sababu ni lazima mrudishe fedha ile iliyowekwa midomoni mwa magunia yenu; pengine ilirudishwa kwa makosa. 13Mchukueni pia ndugu yenu mwende kwa huyo mtu. 14Mungu Mwenye Nguvu na awajalieni kupata huruma mbele ya mtu huyo, awaachieni yule ndugu yenu mwingine na Benyamini warudi pamoja nanyi. Kwa upande wangu, ikinipasa kufiwa na wanangu basi!”
15Hapo, wakachukua zile zawadi, na fedha mara mbili ya zile za awali, wakaenda Misri pamoja na ndugu yao Benyamini. Walipowasili, wakaenda na kusimama mbele ya Yosefu. 16Yosefu alipomwona Benyamini pamoja nao, akamwambia msimamizi wa nyumba yake, “Wapeleke watu hawa nyumbani, umchinje mnyama mmoja na kumtengeneza vizuri, maana watu hawa watakula nami chakula cha mchana.” 17Msimamizi huyo akafanya kama alivyoagizwa: Akawapeleka wale wageni nyumbani kwa Yosefu. 18Walipoona wamepelekwa nyumbani kwa Yosefu, wakashikwa na hofu, wakasema wao kwa wao, “Tumeletwa huku kwa sababu ya ile fedha tuliyorudishiwa katika magunia yetu tulipokuja safari ya kwanza ili apate kisingizio cha kutushambulia ghafla na kutunyanganya punda wetu na kutufanya watumwa wake.” 19Kwa hiyo wakamwendea yule msimamizi wa nyumba ya Yosefu wakaongea naye wakiwa mlangoni, 20wakamwambia, “Samahani, bwana! Sisi tulikuja hapa mara ya kwanza kununua chakula. 21Tulipofika mahali pa kulala wageni huko njiani, tulifungua magunia yetu, tukashangaa kukuta fedha ya kila mmoja wetu mdomoni mwa gunia lake bila kuguswa. Sasa tumeirudisha fedha hiyo. 22Tumeleta na fedha nyingine kununulia chakula. Hatujui ni nani aliyeweka fedha yetu katika magunia yetu.” 23Yule msimamizi akawajibu, “Msiwe na wasiwasi, wala msiogope. Bila shaka Mungu wenu, Mungu wa baba yenu, ndiye aliyewarudishieni fedha katika magunia yenu. Mimi nilipokea fedha yenu.” Kisha akawaletea Simeoni, ndugu yao. 24Huyo msimamizi alipowakaribisha nyumbani kwa Yosefu, akawapa maji ya kunawa miguu yao, na punda wao akawalisha. 25Nao wakatayarisha zawadi zao za kumpa Yosefu, kwa sababu walisikia kuwa watakula pamoja naye.
26Yosefu, aliporudi nyumbani, wakamletea zile zawadi walizokuwa nazo, wakamwinamia kwa heshima. 27Yosefu akawauliza habari zao na kusema, “Mlinisimulia habari za mzee, baba yenu. Je, hajambo? Angali hai?” 28Wakamjibu, “Mtumishi wako, baba yetu, hajambo na angali hai.” Kisha wakainama kwa heshima. 29Yosefu alipoinua macho yake na kumwona Benyamini, nduguye, mtoto wa mama yake, akasema, “Huyu ndiye ndugu yenu mdogo mliyeniambia habari zake? Mungu na akufadhili, mwanangu!” 30Ghafla, Yosefu akatoka mahali hapo, kwani machozi yalikuwa yanamlengalenga kwa shauku kubwa juu ya ndugu yake, akaingia chumbani mwake na kuangua kilio. 31Baada ya kunawa uso wake, alitoka huku akijikaza, akaamuru chakula kiletwe. 32Yosefu aliandaliwa chakula chake peke yake, na ndugu zake wakaandaliwa peke yao, hali kadhalika na Wamisri waliokula pamoja naye, wakaandaliwa peke yao, kwani ni chukizo kwa Wamisri kula chakula pamoja na Waebrania. 33Ndugu zake Yosefu waliketi mbele yake kulingana na umri wao, kuanzia wa kwanza hadi wa mwisho, wakawa wanaangaliana kwa mshangao. 34Chakula kilikuwa kikichukuliwa kutoka mezani pa Yosefu na kupelekwa kwao, lakini Benyamini alipewa mara tano zaidi ya kiasi walichopewa ndugu zake. Basi, wakanywa na kufurahi pamoja naye.
Mwanzo43;1-34

Bible Society of Tanzania

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Friday 17 March 2017

Rais Magufuli afuta agizo la kufunga ndoa kwa sharti la kuwa na cheti cha kuzaliwa




Shukrani;ikulu mawasiliano

"Swahili Na Waswahili"Pamoja Daima.

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo42....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Tumshukuru Mungu kwa Imani na kweli,Yeye aliyetupa kibali cha kuiona leo hii,Mungu wetu yu mwema sana,Yeye aliyetuchagua kwa Mapenzi yake na si kwa wema na nguvu zetu..Kwa Neema/Rehema yeye ametupa pumzi na kuweza kusimama tena..Yeye ni Mwanzo na yeye ni mwisho..

Fadhili zake,Upendo watoka kwake,Furaha na Amani zapatikana kwawe..
Tukiamini na kufuata njia zake kamwe hatutapotea..Eee Mungu utuongoze katika njia zako..

Mitume wakamwambia Bwana, “Utuongezee imani.” Naye Bwana akajibu, “Kama imani yenu ingekuwa ndogo hata kama chembe ndogo ya haradali, mngeweza kuuambia mti huu wa mkuyu: ‘Ngoka ukajipandikize baharini,’ nao ungewatii.
Utubariki na kutulinda katika Kazi zetu,Biashara,Masomo..Tuingiapo/tutokapo,vyombo vya usafiri,Hatua zetu ziwe nawe Mfalme wa Amani,Ukatutakase miili yetu na akaili zetu,Ukavitakase vyote tunavyoenda kugusa/kutumia na Damu ya mwana wako Bwana wetu na mwokozi wetu Yesu Kristo..
Utusamehe pale tulipokwenda kinyume nawe Baba nasi utupe neema ya kuweza kusameheana..
Ukawaguse na kuwaponya Wagonjwa,wanaopitia magumu/mapito,wenye Shida/Tabu na wote walio Magerezani pasipo na hatia...walifungwa kwa minyororo ya mwovu Baba ukawafungue na kuwaweka huru Kiroho na kimwili..
Roho Mtakafu akatuongoze kwenye kunena/kutenda, ukatufanye chombo chema na ukatutumie sawa sawa na mapenzi yako..


Tunajiachilia mikononi mwako Baba wa Mbinguni,Tunashukuru na Kukusifu,Tukiamini wewe ni Bwana na Mwokozi wetu..
Amina...!!
Mungu awabariki.


Ndugu za Yosefu wanakwenda Misri

1Yakobo alipopata habari kwamba kulikuwa na nafaka huko Misri, aliwaambia wanawe, “Mbona mnaketi mkitazamana tu? 2Nimesikia kwamba Misri kuna nafaka. Nendeni huko mkanunue nafaka tusije tukafa njaa.” 3Hivyo ndugu kumi wa Yosefu wakaenda Misri kununua nafaka. 4Lakini Yakobo hakumwacha Benyamini, nduguye Yosefu, aende pamoja nao maana aliogopa kwamba angeweza kupata madhara. 5Basi, wana wa Israeli wakafika Misri wakiwa miongoni mwa wanunuzi wengine, kwani hata katika nchi ya Kanaani kulikuwa na njaa.
6Wakati huo Yosefu alikuwa ndiye mkuu huko Misri. Yeye ndiye aliyehusika na kuwauzia wananchi nafaka. Basi, kaka zake wakaja na kumwinamia Yosefu kwa heshima. 7Yosefu alipowaona kaka zake akawatambua, lakini akajifanya kana kwamba hawafahamu, akasema nao kwa ukali. Akawauliza, “Mmetoka wapi nyinyi?” Wakamjibu, “Tumetoka nchini Kanaani, tumekuja kununua chakula.” 8Ingawa Yosefu aliwatambua kaka zake, wao hawakumtambua. 9Akakumbuka ndoto zake za zamani juu ya kaka zake, akawaambia, “Nyinyi ni wapelelezi. Mmekuja kupeleleza udhaifu wa nchi yetu.” 10Wao wakamjibu, “Sivyo, bwana wetu. Sisi watumishi wako tumekuja kununua chakula. 11Sisi ni ndugu, wana wa baba mmoja. Sisi ni watu waaminifu, na wala si wapelelezi.” 12Lakini Yosefu akasisitiza, “Sivyo! Mmekuja hapa ili kupeleleza udhaifu wa nchi yetu.” 13Wakamwambia, “Sisi, watumishi wako, tuko ndugu kumi na wawili, wana wa mtu mmoja, mwenyeji wa nchi ya Kanaani. Mdogo wetu amebaki na baba nyumbani, na ndugu yetu mwingine ni marehemu.” 14Lakini Yosefu akawaambia, “Ni kama nilivyosema: Nyinyi ni wapelelezi tu. 15Hivi ndivyo mtakavyojaribiwa: Naapa kwa jina la Farao, kwamba hamtatoka hapa mpaka mdogo wenu atakapokuja. 16Mtumeni mmoja wenu akamlete huyo ndugu yenu mdogo, wakati wengine wenu wanamngoja gerezani. Hapo ndipo maneno yenu yatakapojulikana ukweli wake. La sivyo, naapa kwa jina la Farao kwamba nyinyi ni wapelelezi.” 17Kisha akawatia wote gerezani kwa muda wa siku tatu.
18Siku ya tatu Yosefu akawaambia, “Kwa kuwa mimi ni mcha Mungu, fanyeni hivi ili mpate kuishi: 19Kama kweli nyinyi ni watu waaminifu, mmoja wenu na abaki kifungoni, na wengine wawapelekee nafaka jamaa zenu wenye njaa. 20Kisha mleteni kwangu ndugu yenu mdogo. Hii itathibitisha ukweli wa maneno yenu, nanyi hamtauawa.” Basi, wakakubali kufanya hivyo. 21Kisha wakasemezana wao kwa wao, “Kweli sisi tulimkosea ndugu yetu. Ingawa tulimwona akisononeka rohoni mwake, sisi hatukumjali hata alipotusihi. Ndiyo maana taabu hii yote inatupata.” 22Reubeni akawaambia, “Je, mimi sikuwaambieni tusimdhuru kijana? Lakini nyinyi hamkunisikiliza! Sasa tunaadhibiwa kwa ajili ya damu yake.” 23Wao hawakujua kuwa Yosefu alielewa yote hayo waliyosema, maana alipoongea nao ilikuwa kwa njia ya mkalimani. 24Yosefu akaenda kando, akaangua kilio. Alipotulia, akarudi kuzungumza nao. Kisha akamkamata Simeoni na kumtia pingu mbele ya macho yao.

Ndugu za Yosefu wanarudi nyumbani

25Yosefu akatoa amri mifuko yao ijazwe nafaka, kila mmoja wao arudishiwe fedha yake katika gunia lake, na wapewe chakula cha njiani. Wakafanyiwa mambo hayo yote. 26Wakawatwisha punda wao mizigo yao ya nafaka, wakaondoka. 27Ikawa walipofika mahali pa kulala wageni huko njiani, mmoja wao akafungua gunia lake ili apate kumlisha punda wake, akashangaa kukuta fedha yake mdomoni mwa gunia lake. 28Akawaambia ndugu zake, “Fedha yangu imerudishwa. Hii hapa mdomoni mwa gunia langu!” Waliposikia hayo, wakafa moyo. Wakatazamana huku wanatetemeka na kuulizana, “Ni jambo gani hili alilotutendea Mungu?”
29Walipowasili nchini Kanaani kwa baba yao Yakobo, walimsimulia yote yaliyowapata, wakamwambia, 30“Mkuu wa nchi ile alisema nasi kwa ukali, na kutushuku kwamba sisi ni wapelelezi nchini mwake. 31Lakini sisi tulimweleza kuwa sisi ni watu waaminifu, na wala si wapelelezi. 32Tulimweleza kuwa sisi tuko ndugu kumi na wawili wa baba mmoja, na kwamba mmoja wetu ni marehemu na yule mdogo yuko nyumbani nchini Kanaani pamoja na baba yetu. 33Ndipo mkuu wa nchi hiyo akatuambia, ‘Hivi ndivyo nitakavyotambua kama kweli nyinyi ni watu waaminifu: Mwacheni kwangu ndugu yenu mmoja, nanyi wengine mpeleke nafaka nyumbani kwa jamaa zenu wenye njaa. 34Kisha mleteni kwangu huyo ndugu yenu mdogo, na hapo nitajua kuwa nyinyi si wapelelezi, ila ni watu waaminifu. Mkifanya hivyo nitamwacha huru ndugu yenu, nanyi mtaruhusiwa kufanya biashara katika nchi hii.’”
35Walipokuwa wanamimina nafaka kutoka magunia yao, walishangaa kuona kila mmoja wao amerudishiwa kifuko chake na fedha ndani ya gunia lake. Walipoona hayo, wote pamoja na baba yao, wakashikwa na hofu. 36Baba yao Yakobo, akawaambia, “Mnanipokonya watoto wangu! Yosefu hayuko; Simeoni hayuko; sasa mnataka kumchukua na Benyamini. Yote hayo yamenipata!”
37Hapo Reubeni akamwambia baba yake, “Nisipomrudisha Benyamini, waue wanangu wawili. Mwache Benyamini mikononi mwangu, nami nitamlinda na kumrudisha kwako.” 38Lakini baba yake akamjibu, “Mwanangu hatakwenda nanyi; ndugu yake amekwisha fariki, naye peke yake ndiye aliyebaki. Mimi ni mzee mwenye mvi ikiwa kijana huyu atapatwa na madhara yoyote katika safari mtakayofanya basi, mtaniua kwa huzuni.”
Mwanzo42;1-38
Bible Society of Tanzania"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Thursday 16 March 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo41....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Tumshukuru Mungu kwa wema na fadhili zake..

Ni vema kukushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kuliimbia sifa jina lako, ee Mungu Mkuu. Ni vema kutangaza fadhili zako asubuhi, na uaminifu wako nyakati za usiku, kwa muziki wa zeze na kinubi, kwa sauti tamu ya zeze. Ee Mwenyezi-Mungu, matendo yako yanifurahisha; nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda. Matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, ni makuu mno! Mawazo yako ni mazito mno!
Mtakatifu Matakatifu Baba wa Mbinguni, Tunashukuru na kukusifu daima..Asante kwa kibali ulichotupa Baba cha kuiona siku  hii..
Tunaomba ukatubariki katika Kazi zetu,Biashara,Masomo,Vyombo vya usafiri,tutembeapo Baba hatua zetu ziwe nawe..Ukabariki Vilaji/Vinywaji na vyote tunavyoenda kutumia/kugusa Baba wa Mbinguni ukavitakase na Damu ya Mwokozi wetu Bwana wetu Yesu Kristo...
Roho Mtakati akatuongoze katika yote..
Tunakwenda kinyume na mwovu ,Tunakuja mbele zako Baba wa Mbinguni Utusamehe pale tulipokwenda kinyume nawe..
Tupate kiu ya kujua na kujifunza zaidi juu ya Fadhili na wema wako..


Uwaponye na kuwaokoa wote wanaoteseka kwa Magonjwa,Shida/Tabu na vifungo vya mwovu..
Baba Mungu utawale maisha yetu na utupe sawa sawa na mapenzi yako..
Tunayaweka haya mikononi mwako na tukiomba na kushukuru...
Tukiamini wewe ni Bwana wa Majeshi,Mlinzi mkuu,Bwana na Mwokozi wetu..
Amina...!!!!



Mungu aliye chanzo cha amani na awe nanyi nyote! Amina![Waroma 15:33]


Yosefu mbele ya Farao

1Baada ya miaka miwili mizima, Farao aliota ndoto: Alijikuta amesimama kando ya mto Nili, 2akaona ng'ombe saba wazuri na wanono wakitoka mtoni na kula nyasi. 3Halafu, baada ya hao, ng'ombe wengine saba waliokonda sana wakatoka katika mto Nili, wakaja na kusimama karibu na wale ng'ombe wazuri na wanono, kando ya mto. 4Hao ng'ombe waliokonda sana wakawala wale wengine saba wazuri na wanono. Hapo Farao akaamka usingizini. 5Alipolala tena, akaota mara ya pili. Aliona masuke saba makubwa na mazuri yanachipuka katika bua moja. 6Halafu, baada ya hayo, masuke mengine saba membamba na yaliyokaushwa na upepo mkavu wa jangwani yakatokeza. 7Hayo masuke saba membamba yakayameza yale masuke saba makubwa yaliyojaa nafaka. Basi, Farao alipoamka akagundua kuwa ilikuwa ndoto. 8Kulipokuwa asubuhi, Farao akiwa na wasiwasi sana, aliwaita wachawi wote wa Misri, na wenye hekima, akawaambia ndoto zake, lakini hakuna hata mmoja aliyeweza kumtafsiria ndoto hizo.
9Ndipo, yule mtunza vinywaji mkuu akamwambia Farao, “Leo nayakumbuka makosa yangu! 10Wakati ule ulipotukasirikia sisi watumishi wako, mimi na mwoka mikate mkuu, ulitufungia ndani ya ngome ya mkuu wa kikosi cha ulinzi. 11Usiku mmoja tuliota ndoto, kila mmoja ndoto yake tofauti. 12Basi, kijana mmoja Mwebrania, mtumishi wa mkuu wa kikosi cha ulinzi, alikuwa pamoja nasi kifungoni. Tulipomsimulia ndoto zetu, yeye aliweza kututafsiria kila mmoja wetu kulingana na ndoto yake. 13Alivyotafsiri ndivyo ilivyotokea: Mimi nikarudishwa kazini kwangu, na yule mwoka mikate mkuu akatundikwa mtini.”
14Basi, Farao akaamuru Yosefu aitwe; naye akatolewa gerezani haraka. Baada ya kunyoa na kubadili nguo zake, Yosefu akaja mbele ya Farao. 15Farao akamwambia Yosefu, “Mimi nimeota ndoto, lakini hakuna mtu aliyeweza kunitafsiria. Nimesikia sifa zako kwamba wewe ukiambiwa ndoto unaweza kuitafsiri.” 16Yosefu akamjibu Farao, “Sina uwezo huo; lakini Mungu atakupa jibu lifaalo.” 17Hapo Farao akamwambia Yosefu, “Niliota kwamba nimesimama kando ya mto Nili, 18nikaona ng'ombe saba wazuri na wanono wakitoka mtoni na kula nyasi. 19Hao wakafuatwa na ng'ombe wengine saba dhaifu, wembamba na wamekonda sana. Mimi sijapata kamwe kuona ng'ombe wa hali hiyo katika nchi ya Misri. 20Basi, wale ng'ombe waliokonda sana wakawala wale ng'ombe saba wanono. 21Lakini hata baada ya kuwala wale wanono, mtu yeyote asingeweza kutambua kwamba wamewala wenzao, kwani bado walikuwa wamekondeana kama mwanzo. Hapo nikaamka usingizini. 22Kisha nikaota ndoto nyingine: Niliona masuke saba mazuri yaliyojaa nafaka yakichipua katika bua moja. 23Halafu yakafuatwa na masuke mengine saba matupu, membamba na yaliyokaushwa na upepo mkavu wa jangwani. 24Yale masuke saba membamba yakayameza yale masuke saba mazuri. Basi, mimi niliwaambia wachawi ndoto hizo lakini hakuna mtu aliyeweza kunifafanulia.”
25Ndipo Yosefu akamwambia Farao, “Ndoto zako zote mbili tafsiri yake ni moja. Mungu amekufunulia mambo atakayofanya hivi karibuni. 26Ngombe wale saba wazuri ni miaka saba, na yale masuke saba mazuri pia ni miaka saba; ndoto hiyo tafsiri yake ni moja. 27Wale ng'ombe saba waliokonda sana, ambao waliwafuata wale wanono, na yale masuke matupu saba, yaliyokaushwa na upepo mkavu wa jangwani, maana yake ni miaka saba ya njaa. 28Kama nilivyokueleza, ee Farao, Mungu amekufunulia mambo atakayofanya hivi karibuni. 29Kutakuwa na miaka saba ya shibe katika nchi nzima ya Misri. 30Lakini baadaye itafuata miaka saba ya njaa, hata hiyo shibe isahaulike kabisa. Njaa hiyo itaiangamiza nchi hii. 31Shibe hiyo itasahaulika kabisa kwa sababu njaa itakayofuata itakuwa kali mno. 32Ndoto yako ilirudiwa mara mbili kwa mifano inayofanana kukuonesha kwamba Mungu ameamua, naye atatekeleza jambo hilo karibuni.
33“Kwa hiyo yafaa sasa, ee Farao, umteue mtu mwenye ujuzi na hekima, umpe jukumu la kuiangalia nchi yote ya Misri. 34Tena, ee Farao, uwateue wasimamizi kadhaa hapa nchini, uwaagize wakusanye sehemu ya tano ya mavuno yote ya Misri katika kipindi hiki cha miaka saba ya shibe. 35Uwaagize wasimamizi hao wakusanye chakula chote katika miaka saba ijayo ya mavuno kwa wingi. Nafaka hiyo na iwekwe chini ya mamlaka yako, ee Farao, iwe akiba ya chakula kwa miji yote, nao waitunze nafaka hiyo. 36Chakula hicho kitakuwa akiba ya kinga kwa nchi ya Misri isije ikaangamia kutokana na njaa ya miaka saba itakayofuata.”

Yosefu apewa cheo

37Shauri alilotoa Yosefu lilionekana kuwa jema mbele ya Farao na watumishi wake wote. 38Kwa hiyo Farao akawauliza watumishi wake, “Huyu mtu ana roho ya Mungu! Je, tunaweza kumpata mtu mwingine kama huyu?” 39Kisha akamwambia Yosefu, “Kwa kuwa Mungu amekufunulia haya yote, hakuna mtu mwingine mwenye busara na hekima kama wewe. 40Wewe ndiwe utakayeisimamia nchi yangu, na watu wangu wote watakuwa chini ya amri yako. Mimi tu ndiye mkuu kuliko wewe kwa kuwa nakalia kiti cha kifalme. 41Basi, sasa nakuteua rasmi kuwa mkuu wa nchi yote ya Misri!” 42Ndipo, Farao akaivua pete yake ya mhuri kidoleni mwake na kumvisha Yosefu, akamvalisha na mavazi ya kitani safi na mkufu wa dhahabu shingoni. 43Farao akampandisha katika gari lake la pili la farasi na walinzi wakatangulia mbele ya Yosefu wakipaza sauti na kusema, “Pigeni magoti!” Ndivyo Farao alivyompa Yosefu madaraka makubwa juu ya nchi yote ya Misri. 44Zaidi ya hayo, Farao akamwambia Yosefu, “Mimi ndimi Farao! Nasema: Mtu yeyote katika nchi nzima ya Misri asiinue mkono wala mguu wake bila kibali chako.” 45Farao akampa Yosefu jina la Kimisri: Safenath-panea. Akamwoza Asenathi binti Potifera, kuhani wa mji wa Oni. Basi, Yosefu akaanza kuitembelea nchi nzima ya Misri.
46Yosefu alikuwa na umri wa miaka thelathini alipoanza kumtumikia Farao, mfalme wa Misri. Alitoka nyumbani kwa Farao na kuitembelea nchi yote ya Misri. 47Ikawa, katika miaka ile saba ya shibe, mashamba ya Misri yakatoa mazao kwa wingi sana. 48Yosefu akakusanya chakula chote wakati huo wa miaka saba ya shibe na kukiweka akiba katika miji ya Misri. Katika kila mji akaweka akiba ya chakula kutoka mashamba yaliyo karibu na mji huo. 49Yosefu akaweka akiba ya nafaka kwa wingi mno ikawa nyingi kama mchanga wa bahari, hata isiweze kupimika.
50Kabla ya miaka ya njaa kuanza, Yosefu alikuwa amekwisha pata wana wawili kwa mkewe, Asenathi, binti Potifera, kuhani wa mji wa Oni. 51Yosefu alimwita mwanawe wa kwanza Manase, akisema, “Mungu amenifanya nisahau taabu zangu zote na jamaa ya baba yangu.” 52Mwanawe wa pili akamwita Efraimu, akisema, “Mungu amenipa watoto katika nchi ya mateso yangu.”
53Miaka ile saba ya shibe nchini Misri ikapita. 54Ikaanza miaka saba ya njaa kama alivyokuwa amesema Yosefu hapo awali. Nchi nyingine zote zikawa na njaa, lakini nchi yote ya Misri ilikuwa na chakula. 55Wakati wananchi wa Misri walipoanza kuona njaa, walimlilia Farao awape chakula. Naye Farao akawaambia Wamisri wote, “Nendeni kwa Yosefu; atakalowaambia fanyeni.” 56Njaa ikazidi kuwa kali na kuenea katika nchi yote. Kwa hiyo Yosefu akazifungua ghala zote, akawauzia Wamisri chakula. 57Zaidi ya hayo, watu toka kila mahali duniani walikuja Misri kwa Yosefu kununua nafaka, kwani njaa ilikuwa kali duniani kote.
Mwanzo41;1-57

Bible Society of Tanzania
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.

Wednesday 15 March 2017

Kikombe Cha Asubuhi;Mwanzo40....

Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje Wapendwa/Waungwana?
Tunamshukuru Mungu mkuu kwa Matendo yake makuu,Muumba wetu,Muumba Mbingu na Nchi,Muweza wa yote,Hakuna wa kufanana naye,Yeye ni mwanzo na yeye ni mwisho,Hakuna lisilowezekana mbele zake Mungu..Yeye ndiye aliyetupa kibali cha kuiona leo hii..Yeye ndiye alituchagua tena..Tumsifu Mungu wetu na kumtukuza daima..Yeye anatujua zaidi tunavyojijua..shukrani na utukufu ni kwake Muumba wetu..
Tazama Jana imepita Mungu wetu,Leo ni siku mpya,Kesho ni siku nyingine Baba Mungu..Utubariki tuingiapo/tutokapo,hatua zetu ziwe na we Baba wa Mbinguni,Ubariki kazi zetu Baba..Biashara,Masomo,Vilaji/Vinywaji,Vyombo vya usafiri na tutembeapo...Ukavitakase vyote tunavyoenda kuvitumia/kugusa Mfalme wa Amani..Roho Mtakatifu akatuongoze kwenye kunena/Kutenda,Ukatufanye chombo chema na ukatutumie sawasawa na mapenzi yako..Ukabariki Ridhiki zetu Baba wa mbinguni..kinachoingia na kutoka...
Utusamehe pale tulipokwenda kinyume nawe Mwokozi..
Utupe Neema ya kuweza kusameheana Baba wa mbinguni..

Baba Mungu ukaibariki Nchi hii tunayoishi,Ukabariki pia Tanzania,Afrika na Dunia yote Mfalme wa Amani ukatawale..Ukawaongoze wanaotuongoza na wakatuongoze katika haki na kweli..

Baba ukawaponye na kuwaokoa wote wanaopitia Magumu/Majaribu,Shida/Tabu zozote..Ukawafungue waliokwenye vifungo vya mwovu.. wapate kupona kiroho na kimwili Baba..
Tunajiachilia mikononi mwako Baba wa Mbingu Tukiamini wewe ni Bwana na Mwokozi wetu.. Amina..!!!!

Muwe na Wakati mwema.


Yosefu anatafsiri ndoto

1Wakati fulani baada ya mambo hayo, maofisa wawili wa mfalme wa Misri walimkosea mfalme. Maofisa hao walikuwa mtunza vinywaji mkuu na mwoka mikate mkuu wa mfalme. 2Farao aliwakasirikia hao maofisa wake wawili, 3akawafungia ndani ya ngome ya mkuu wa kikosi cha ulinzi, katika gereza, mahali alipofungwa Yosefu. 4Mkuu wa kikosi cha ulinzi akamteua Yosefu awatumikie. Nao wakawa kifungoni kwa muda fulani.
5Basi, usiku mmoja, yule mtunza vinywaji mkuu na yule mwoka mikate mkuu wa mfalme wa Misri, waliota ndoto humo gerezani, kila mmoja na ndoto yake tofauti. 6Yosefu alipokwenda kwao asubuhi na kuwaona, wote wawili walikuwa wenye wasiwasi. 7Basi, Yosefu akawauliza maofisa hao wa Farao waliokuwa kifungoni pamoja naye nyumbani mwa bwana wake, “Mbona leo mna nyuso za huzuni?” 8Wakamjibu, “Tuna huzuni kwa kuwa tumeota ndoto na hakuna awezaye kututafsiria ndoto zetu.” Yosefu akawaambia, “Je, kutafsiri ndoto si kazi ya Mungu? Basi, niambieni ndoto zenu.”
9Mtunza vinywaji mkuu wa mfalme akamsimulia Yosefu ndoto yake, akisema, “Katika ndoto yangu niliona mzabibu mbele yangu, 10nao ulikuwa na matawi matatu. Mara tu ulipoanza kuchipua majani, maua yake yalichanua na vishada vyake vikawa zabibu mbivu. 11Mkononi mwangu nilikuwa na kikombe cha Farao, basi, nikazitwaa zabibu, nikazikamua katika kikombe hicho, nikampa Farao.” 12Yosefu akamwambia huyo mtumishi, “Tafsiri ya ndoto yako ni hii: Yale matawi matatu ni siku tatu. 13Baada ya siku tatu Farao atakunyanyua kutoka gerezani na kukurudisha tena katika cheo chako. Utaweza tena kumpa Farao kikombe mkononi kama ulivyokuwa unafanya hapo awali. 14Lakini tafadhali usinisahau wakati mambo yatakapokwendea vema; unifanyie fadhili na kunitaja mbele ya Farao, nipate kutoka humu gerezani. 15Maana mimi nilitoroshwa kutoka nchi ya Waebrania, na hapa Misri sijafanya chochote kinachostahili nitiwe gerezani.”
16Yule mwoka mikate mkuu alipoona kwamba tafsiri ile ni nzuri, akamwambia Yosefu, “Hata mimi niliota ndoto! Katika ndoto yangu nilikuwa nimechukua kichwani nyungo tatu za mikate. 17Katika ungo wa juu, kulikuwa na vyakula mbalimbali vilivyookwa kwa ajili ya Farao. Lakini, ndege walikuwa wakivila kutoka ungo huo kichwani pangu!” 18Yosefu akamwambia, “Tafsiri ya ndoto yako ni hii: Zile nyungo tatu ni siku tatu. 19Baada ya siku tatu Farao atakunyanyua kutoka gerezani, atakiinua kichwa chako akutundike mtini, nao ndege wataula mwili wako.”
20Mnamo siku ya tatu, ambayo ilikuwa siku ya kuadhimisha kuzaliwa kwake, Farao aliwaandalia karamu watumishi wake wote. Akawatoa gerezani mtunza vinywaji wake mkuu na mwoka mikate mkuu, akawaweka mbele ya maofisa wake. 21Kisha akamrudishia cheo chake mtunza vinywaji, apate kumpatia Farao kikombe. 22Lakini yule mwoka mkate mkuu akamtundika mtini, kama Yosefu alivyokuwa amewatafsiria ndoto zao. 23Hata hivyo, yule mtunza vinywaji mkuu akamsahau Yosefu, badala ya kumkumbuka.
Mwanzo40;1-23

Bible Society of Tanzania
"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.