Swahili na Waswahili

Swahili na Waswahili
Waswahili na Mswahili Rachel Siwa...Pamoja Daima!!

Friday 6 October 2017

Kikombe Cha Asubuhi Kumbukumbu la Sheria 33 (Kumbukumbu la Torati katika tafsiri nyingine)



Shalom,Habari za Asubuhi,Hamjambo,Mmeamkaje?

Tumshukuru Mungu wetu kwa Mema mengi aliyotutendea/anayotutendea

Mtakatifu Baba wa Mbinguni,Mungu wetu ,Baba yetu..
Muumba wetu,Muumba wa vyote,Mwenyezi-Mungu shujaa vitani
Mwenyezi-Mungu muweza wa yote,Mwenyezi-Mungu mwenye huruma,Mwenyezi-Mungu ndiye mponyaji,Mwenyezi-Mungu ndiyo jina lake..



Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia mara nyingine, wakati alipokuwa bado amefungwa katika ukumbi wa walinzi: Mwenyezi-Mungu aliyeiumba dunia, Mwenyezi-Mungu aliyeifanya na kuiimarisha dunia, ambaye jina lake ni Mwenyezi-Mungu, aliniambia, “Niite, nami nitakujibu na kukuambia mambo makubwa yaliyofichika ambayo hujapata kuyajua. Maana, mimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, nasema kwamba nyumba za mji wa Yerusalemu na nyumba za wafalme wa Yuda zitabomolewa kwa sababu ya kuzingirwa na kwa sababu ya mashambulizi. Watu watajaribu kuwakabili Wakaldayo lakini hiyo itakuwa bure, maana mahandaki yatajaa maiti za watu ambao nitawaua kwa hasira na ghadhabu yangu. Kwa vile wamefanya uovu huo wote, mimi nitauacha mji huu. “Hata hivyo, mimi nitauponya mji huu na kuwapa watu wake afya; nitawajalia ustawi mwingi na usalama. Nitawastawisha tena watu wa Yuda na watu wa Israeli; nitawaimarisha kama walivyokuwa hapo awali. Nitawatakasa dhambi zao zote na kuwasamehe uovu wao na uasi walionitendea. Nao mji huu utakuwa sababu ya furaha kwangu, mji wa sifa na fahari mbele ya mataifa yote duniani ambayo yatasikia juu ya mema yote ninayowafanyia. Mataifa yataogopa na kutetemeka kwa sababu ya mema na fanaka nitakazouletea mji huu wa Yerusalemu.” Mwenyezi-Mungu asema: “Katika mji huu ambao mnasema umekuwa ukiwa bila watu wala wanyama, naam, katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu ambazo ni tupu, bila watu wala wanyama, humo kutasikika tena sauti za vicheko, sauti za furaha, sauti za harusi na za furaha, sauti za waimbaji wakati wakileta tambiko za shukrani katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu: ‘Mshukuruni Mwenyezi-Mungu wa majeshi kwa kuwa Mwenyezi-Mungu ni mwema, kwa maana fadhili zake zadumu milele.’ Nitairudishia nchi hii fanaka yake ya awali. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”


Asante Baba wa Mbinguni kwa wema na fadhili zako kwetu..
Asante kwa ulinzi wako wakati wote..
Asante kwakutuchagua tena na kutupa kibali cha kuendelea kuiona leo hii..
Utukuzwe Mungu wetu,Uhimidiwe Baba wa Mbinguni..
Unastahili sifa,Unastahili kuabudiwa Mwenyezi-Mungu..
Baba wa Upendo,Baba wa baraka,Baba wa yatima,Mume wa wajane..
Sifa na Utukufu tunakurudishia wewe..



Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Mahali hapa ambapo ni jangwa bila watu wala wanyama, na katika miji yake yote, patakuwa na malisho ambayo wachungaji watalisha makundi yao ya kondoo. Katika miji ya nchi yenye milima, katika miji ya Shefela na katika miji ya jangwa la Negebu, katika nchi ya Benyamini, kandokando ya mji wa Yerusalemu na katika miji ya Yuda, watu watahesabu tena kondoo wao. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.” Mwenyezi-Mungu asema: “Siku zaja ambapo nitatimiza ahadi yangu niliyofanya na watu wa Israeli na watu wa Yuda. Katika siku hizo, naam, wakati huo, nitachipusha chipukizi mwadilifu wa uzao wa Daudi. Chipukizi huyo atatekeleza haki na uadilifu katika nchi. Wakati huo nchi ya Yuda itaokolewa na mji wa Yerusalemu utakuwa salama. Na mji huo utaitwa ‘Mwenyezi-Mungu ni Ukombozi Wetu’. Maana mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Hapatakosekana kamwe mzawa wa Daudi atakayetawala Israeli. Kadhalika nao makuhani wa ukoo wa Lawi watakuwapo daima kunihudumia wakinitolea sadaka za kuteketezwa na sadaka za nafaka na kunitolea tambiko milele.”

Yahweh tunakuja mbele zako tukijinyenyekeza,tukijishusha
na tukijiachilia mikononi mwako Mungu wetu..
Tunaomba utusamehe makosa yetu yote tuliyoyafanya
kwakunena,kwakutenda,kwakujua/kutojua..
Mfalme wa Amani nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
 kuwasamehe wale wote waliotukosea..
Mungu wetu utuepushe katika majaribu na utuokoe
 na yule mwovu na kazi zake zote..
Baba wa Mbinguni tunaomba ututakase miili yetu
 na akili zetu Jehovah utufunike kwa Damu ya Bwana wetu
Yesu Kristo wa Nazareti,yeye aliteseka kwanza ili sisi tupate kupona..

Mwenyezi-Mungu tunaomba ukabariki kazi za mikono yetu
Biashara,masomo na vyote tunavyoenda kufanya/kutenda 
Baba wa Mbinguni tukatende kama inavyokupendeza wewe..
Jehovah tunaomba ukabariki ridhiki zetu ziingiazo/zitokazo
Mungu wetu nasi tunaomba utupe neema ya kuweza
 kuwabariki wenye kuhitaji..
Yahweh tusipungukiwe katika mahitaji yetu..
Jehovah ukatupe sawasawa na mapenzi yako..


Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia: “Kama vile hamwezi kutangua agano langu nililoweka kuhusu usiku na mchana hivyo kwamba usiku na mchana visiweko kama nilivyopanga, vivyo hivyo hamwezi kutangua agano langu nililofanya na mtumishi wangu Daudi. Nilifanya agano na Daudi kwamba daima atakuwa na mzawa wa kutawala mahali pake; vilevile kutakuwako daima makuhani wa ukoo wa Lawi watakaonitumikia. Kama vile nyota angani na mchanga wa pwani visivyohesabika, ndivyo nitakavyoongeza idadi ya wazawa wa mtumishi wangu Daudi na idadi ya makuhani wa ukoo wa Lawi.”
Mfalme wa Amani tunaomba amani yako ikatawale katika 
Nyumba/ndoa zetu,watoto,wazazi wetu,familia/ndugu 
na wote wanaotuzunguka..
Mungu wetu tunaomba ulinzi wako wakati wote tuingiapo/tutokapo
Baba wa Mbinguni ukabariki na kuvibariki vyote tunavyoenda
kugusa/kutumi Yahweh ukavitakase na kuvifunika kwa 
Damu ya Mwokozi wetu Yesu Kristo wa Nazareti..
Mungu wetu ukawaguse wote walio katika shida/tabu
wanaopitia magumu/majaribu mbalimbali..
Mungu wetu ukawaponye kimwili na kiroho na ukawarudishe wale waliopote,Mungu wetu ukatupe neema ya kusimamia
Neno lako Amri na Sheria zako siku zote za maisha yetu
Baba wa Mbinguni tukawe barua njema na tukasomeke
kama inavyokupendaza wewe..

Neno la Mwenyezi-Mungu lilimjia Yeremia: “Je, hujasikia wasemayo watu hawa, kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nimewatupilia mbali watu wa Israeli na watu wa Yuda, jamaa mbili nilizoziteua? Wamewadharau watu wangu, hata kuwaona kwamba wao si taifa. Lakini mimi Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Mimi niliweka agano kuhusu mchana na usiku na kuweka sheria za mbingu na dunia. Basi, ndivyo ilivyo pia: Sitawatupa wazawa wa Yakobo na Daudi, mtumishi wangu; nitamteua mmoja wa wazawa wake atawale wazawa wa Abrahamu, Isaka na Yakobo. Kwa maana nitawarudishia fanaka yao na kuwahurumia.”

Roho Mtakatifu akatuongoze katika yote na tuwe na hekima
busara,wanyenyekevu, upole na kiasi..
Ee Mungu wetu tunaomba ukapokee sala/maombi yetu...
Mwenyezi-Mungu Mungu wetu tunakushukuru na
 kuamini kwama wewe ni Mungu wetu leo,kesho na hata milele
Kwakuwa Ufalme ni wako Nguvu na Utukufu hata Milele..
Amina..!
Asanteni sana wapendwa katika Bwana kwakuwa nami
Mwenyezi-Mungu Mungu wa Rehema na Baraka
akawe nanyi daima Amani yake ikatawale katika maisha yenu..
Nawapenda.



Mose anayabariki makabila ya Israeli

1Hii ndiyo baraka ambayo Mose, mtu wa Mungu aliwatakia Waisraeli kabla ya kufariki kwake. Alisema:
2Mwenyezi-Mungu alikuja kutoka mlima Sinai,
alitutokea kutoka mlima Seiri;
aliiangaza kutoka mlima Parani.
Alitokea kati ya maelfu ya malaika,
na moto uwakao katika mkono wake wa kulia.
3Mwenyezi-Mungu aliwapenda watu wake;
na huwalinda watakatifu wake wote.
Hivyo, malaika wake walifuata nyayo zake,
na kupata maagizo kutoka kwake.
4Mose alituamuru tutii sheria;
kitu cha thamani kuu cha taifa letu.
5Mwenyezi-Mungu akawa mfalme wa Israeli,
wakati viongozi wao walipokutana,
na makabila yote yalipokusanyika.
6Mose alisema juu ya kabila la Reubeni:
“Reubeni aishi wala asife,
na watu wake wasiwe wachache.”
7Juu ya kabila la Yuda alisema:
“Ee Mwenyezi-Mungu usikilize kilio cha kabila la Yuda;
umrudishe tena kwa watu wale wengine.
Upigane kwa mikono yako kwa ajili yake,
ulisaidie kabila la Yuda dhidi ya adui zake.”
8Juu ya kabila la Lawi, alisema:
“Ee Mwenyezi-Mungu ulipatie Lawi kauli yako ya Urimu,
kauli yako ya thumimu33:8 kauli yako … kauli yako: Kiebrania: Urimu, Thumimu. Taz Kut 28:30 kwa hao waaminifu wako,
ambao uliwajaribu huko Masa.
9Ulishindana nao kwenye maji ya Meriba.
Walawi walioamua kuwaacha wazee wao,
wakawasahau jamaa zao,
wasiwatambue hata watoto wao
maana walizingatia amri zako,
na kushika agano lako.
10Na wawafundishe wazawa wa Yakobo maagizo yako;
wawafundishe watu wa Israeli sheria yako.
Walawi na wafukize ubani mbele yako,
sadaka nzima za kuteketezwa madhabahuni pako.
11Ee Mwenyezi-Mungu, uzibariki nguvu zao,
uzikubali kazi za mikono yao;
uzivunjilie mbali nguvu za maadui zao,
nguvu za wanaowachukia hata wasiinuke tena.”
12Juu ya kabila la Benyamini alisema:
“Hili ni kabila alipendalo Mwenyezi-Mungu,
nalo hukaa salama karibu naye.
Yeye hulilinda mchana kutwa,
na kukaa kati ya milima33:12 milima: Neno kwa neno: Mabega. yake.”
13Juu ya kabila la Yosefu alisema:
“Mwenyezi-Mungu na aibariki nchi yake,
kwa baraka nzuri kabisa kutoka juu,
14ibarikiwe kwa matunda bora yalioiva kwa jua,
kwa matunda ya kila mwezi;
15kwa mazao bora ya milima ya kale,
na mazao tele ya milima ya kale,
16Nchi yake ijae yote yaliyo mema,
ibarikiwe kwa wema wa Mwenyezi-Mungu,
ambaye alitokea katika kichaka.
Baraka hizi ziwashukie watu wa kabila la Yosefu,
aliyekuwa mkuu miongoni mwa ndugu zake.
17Fahari yake ni fahari ya fahali wa kwanza,
pembe zake ni za nyati dume.
Atazitumia kuyasukuma mataifa;
yote atayasukuma mpaka miisho ya dunia.
Efraimu atakuwa na pembe hizo 10,000
na Manase kwa maelfu.”
18Juu ya kabila la Zebuluni na kabila la Isakari, alisema,
“Zebuluni, furahi katika safari zako;
nawe Isakari, furahi katika mahema yako.
19Watawaalika wageni kwenye milima yao,
na huko watu watatoa sadaka zinazotakiwa.
Maana wao watapata utajiri wao kutoka baharini
na hazina zao katika mchanga wa pwani.”
20Juu ya kabila la Gadi, alisema:
“Atukuzwe Mungu ampatiaye Gadi sehemu kubwa.
Gadi hunyemelea kama simba
akwanyue mkono na utosi wa kichwa.
21Alijichagulia eneo zuri kuliko yote,
mahali ilipotengwa sehemu ya kiongozi.
Aliwaongoza watu na kumtii Mwenyezi-Mungu,
alitekeleza mpango wa Mungu kwa Israeli.”
22Juu ya kabila la Dani alisema hivi:
“Dani ni mwanasimba
arukaye kutoka Bashani.”
23Juu ya kabila la Naftali alisema:
“Ee Naftali fadhili,
uliyejaa baraka za Mwenyezi-Mungu,
nchi yako ni kusini kwenye ziwa Kinerethi.”
24Juu ya kabila la Asheri alisema:
“Asheri abarikiwe kuliko watoto wote wa Yakobo,
na upendelewe na ndugu zako wote;
na achovye mguu wake katika mafuta.
25Miji yako ni ngome za chuma na shaba.
Usalama wako utadumu maisha yako yote!”
26Mose akamalizia kwa kusema,
“Ee Israeli, hakuna aliye kama Mungu wako,
yeye hupita mbinguni kuja kukusaidia,
hupita juu angani katika utukufu wake.
27Mungu wa milele ndiye kimbilio lenu;
nguvu yake yaonekana duniani.
Aliwafukuza maadui mbele yenu;
aliwaamuru: ‘Waangamizeni.’
28Kwa hiyo, watu wa Israeli wakakaa salama,
wazawa wa Yakobo peke yao,
katika nchi iliyojaa nafaka na divai,
nchi ambayo anga lake hudondosha umande.
29Heri yenu nyinyi Waisraeli.
Nani aliye kama nyinyi, watu mliookolewa na Mwenyezi-Mungu,
ambaye ndiye ngao ya msaada wenu,
na upanga unaowaletea ushindi!
Adui zenu watakuja wananyenyekea mbele yenu,
nanyi mtawakanyaga chini.”


Kumbukumbu la Sheria 33:1-29


Biblia Habari Njema kwa Watu Wote(BHN)

"Swahili Na Waswahili"Mbarikiwe.


No comments: